Mali: Serikali yatangaza kusitisha vita
Imechapishwa: Imehaririwa:
Baada ya kuchukua jitihada ya kuanzisha mashambulizi ya kijeshi ili kuurejesha mji wa Kidal kwenye himaya ya seriakli, wanajeshi wa Mali wametimuliwa jumatano ya wiki katika mji huo na makundi ya wapiganaji ya MNLA, MAA pamoja na HCUA. Wakati huohuo serikali ya Mali imetangaza “kusitisha mapigano mara moja”.
Jeshi la Mali lilianza mashambulizi hayo iliyoyaita “ operesheni ya kulinda mali na raia”, kulingana na taarifa iliyotolewa na waziri wa ulinzi. Uamzi wa kuanzisha mashambulizi hayo ulichukuliwa na serikali ya Bamako bila hata hivo kufahamisha na kushirikisha uongozi wa kikosi cha Ufaransa “Serval” na ofisi ya Umoja wa Mataifa nchini Mali Minusma, chanzo cha Umoja wa Mataifa kimefahamisha.
Wanajeshi wa Mali “walikua na imani kwamba watashinda vita hivyo, baada ya kubaini kwamba wana silaha za kutosha kwa kuyatimua makundi ya wapiganaji katika mji wa Kidal”, mwanajeshi mmoja alieshiriki katika mapigano hayo alielezea RFI. Lakini saa chache baada ya kuanzisha mapigano, “uongozi wa jeshi ulisalimu amri na kuamuru wanajeshi kurudi nyuma”. Kwa mujibu wa shahidi huyo, “wanajeshi wa Mali wameelemewa na baadae kushindwa kujidhatiti vilivyo katika vita hivyo”. Baadhi walitimka kwa kutumia magari na wengine kwa kutumia uwezo waliyo kuwa nao. “Nilishuhudia baadhi miili ya wanajeshi waliouawa akiwemo kanali Fayçal Ag Kiba, ambae alikua mshirika wa karibu wa mkuu wa majeshi ya El Hadj Ag Gamou” amesema shahidi huyo.
Makundi ya wapiganaji yalikua tayari kujibu mashambulizi hayo yaliyoanzishwa na jeshi la Mali. Katika muda wa saa kadhaa wapiganaji waliendelea kudhibiti mji huo na kuwatimua wanajeshi, hukua kundi la wapiganaji la MNLA likiweka bendera yake katika kambi moja ya jeshi la Mali. Baadhi ya wanajeshi waliondoka katika mji wa Kidali na kujielekeza katika mji wa Gao, na wengine ambao idadi yao ilikua kubwa walikimbilia katika eneo wanako piga kambi wanajeshi wa kikosi cha Ufaransa “Serval” na wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa.
Mapema jana mchana zaidi ya wanajeshi 40 walikimbilia katika eneo hilo. Hapo jana jioni kundi la MNLA limefahamisha kwamba limekua likiwasiliana na kikosi cha Umoja wa Mataifa pamoja na uongozi wa kikosi cha Ufaransa “Serval” kinachohitajika kufanya.
Hayo yakijiri, serikali ya Mali imetangaza kusitisha mapigano dhidi ya makundi hayo. Kwa mujibu wa tangazo liliosomwa na msemaji wa serikali, Mahamane Baby, kupitia televisheni ya serikali ORTM, jeshi la Mali lilikabiliwa na matatizo mengi mkiwemo ukosefu wa mawasiliano na kusababisha kushindwa katika mapigano.
Jeshi la Ufaransa ambalo lilipunguza idadi ya wanajeshi wake nchini Mali, limetangaza kuwatuma nchini Mali wanajeshi wake zaidi ya mia moja wakitokea nchini Côte d'Ivoire, kanali Gilles Caron, afisa wa gazi ya juu katika jeshi la Ufaransa amesema. Idadi ya wanajeshi wa Ufaransa nchini Mali itafikia kwa sasa 1700.