Burundi: mwanaharakati wa haki za binadamu asalia jela
Mahakama kuu ya Bujumbura imeamru kiongozi wa shirika la kutetea haki za binadamu na za wafungwa nchini Burundi APRODH, Pierre-Clavery Mbonimpa aendelee kukaa korokoroni, wanasheria wake wanajiandaa kukata rufaa dhidi yauamzi huo.
Imechapishwa:
Pierre-Claver Mbonimpa alikamatwa, baada ya kuitishwa mahakamani mara moja ili kujibu mashitaka yanayomkabili ambayo yanahusiana na kuwapa silaha vijana wa chama tawala Cndd-fdd "Imbonerakure", ambapo serikali ilinyooshewa kidole na taasisi za Umoja wa Mataifa kuhusika na kitendo hicho.
Hivi karibuni Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilionya serikali ya Burundi kuachana na kuwapa silaha vijana wa chama tawala, na lilitishia kuwafikisha mbele ya mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita viongozi na raia wengine watakaohusika na kuchochea machafuko kabla, katika na baada uchaguzi nchini Burundi, chaguzi ambazo zinatarajiwa kufanyika mwakani.
Serikali ya Burundi ilikanusha tuhuma hizo dhidi yake, na kuapa kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria waliohusika na kuzagaza habari zisiyokua za kweli ambazo zinapaka tope serikali.
Mashirika ya kiraia na wanaharakati wa haki za binadamu wa Burundi na kungineko duniani wamekua wakiomba Pierre-Claver Mbonimpa achiliwe huru, wakidai kwamba hana hatia yoyote, bali ni ubabe unaoendeshwa na utawala wa Pierre Nkurunziza ili kuwatia uoga wanaharakati wa haki za binadamu wasiendelei kutaja uhalifu unaotendwa na serikali ya Bujumbura dhidi ya raia.