UN: Mapigano Tripoli yameua watu 56
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, mapigano yanayoendeshwa na majeshi ya ANL chini ya amri ya Marshal Khalifa Haftar dhidi ya vikosi vya serikali inayotambuliwa na Jumuiya ya kimataifa, katika viunga vya Tripoli , mji mkuu wa Libya, yameua watu 56.
Majeshi ya Marshal Haftar yanayodhibiti mashariki mwa Libya, yanashikila maeneo kadhaa, kilomita 11 kusini na kati mwa mji mkuu Tripoli.
Miongoni mwa watu waliouawa ni madaktari wawili na msaidizi mmoja wa afya, Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema katika taarifa, bila kueleza ikiwa watu wengine waliouawa ni raia au wapiganaji.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, mapigano kati ya majeshi ya ANL na vikosi vya serikali inayoungwa mkono na Jumuiya ya kimataifa (GNA) yamesababisha maelfu ya waakazi wa viunga vya mji mkuu Tripoli kutoroka makaazi yao.