Haysom: Tunashikamana na AU kuhakikisha utawala wa kiraia unarejea Sudan
Imechapishwa:
Umoja wa Mataifa unashikamana na Muungano wa afrika AU, katika kuhakikisha utawala wa kiraia unarejea nchini Sudan, amesema mshauri maalumu wa Umoja wa Mataifa kwa ajili ya mgogoro mpya wa saudan Nicholas Haysom.
Kauli hii imekuja saa chache baada ya pande kinzani nchini Sudan kutia siani kwenye makubaliano ya kisiasa.
Majadiliano zaidi yataendelea Ijumaa Julai 19 wiki hii katika masuala nyeti ambayo ni “kukubaliana kuhusu azimio la katiba ya mpito ambayo itaamua mfumo wa kushirikiana madaraka kati ya Baraza la Kijeshi na muungano wa makundi ya waandamanaji, ikiwemo mfumo wa vyombo vya utawala na ni kutathimini asilimia ngapi iende kwa kila upande katika baraza la rais.”
Bwana Haysom amesema “Sudan imepitia madhila mengi na hivi sasa ipo katika kipindi muhimu cha mpito cha kuwahakikishia watu wake, ulimwengu na jumuiya ya kimataifa kwamba inataka amani, utulivu na mustakabali bora ambayo ndio matakwa ya wengi ikiwemo ukanda mzima”.
Hivi karibuni Umoja wa Afrika AU, uliweka bayana masuala manne ya kutekeleza na kusema kwamba Sudan itasitishwa uanachama wa AU na mfumo wake endapo haitorejesha utawala kwa serikali ya kiraia.