DRC-Mpango wa dharura wa siku 100: Vital Kamerhe akanusha tuhuma dhidi yake
Imechapishwa:
Aliyekuwa mnadhimu mkuu katika Ofisi ya rais jijini Kinshasa Vital Kamerhe amekanusha madai ya kutumia vibaya zaidi ya dola milioni 50 za Kimarekani zilizokuwa zimetengwa kugharamia ujenzi wa makaazi ya polisi na maafisa wa jeshi jijini Kinshasa wakati kesi yake iliporejelewa Jumatatu Mei 25.
Akijibu baadhi ya maswali ya majaji kuhusu mikataba ya ununuzi wa nyumba kutoka kampuni ya Samibo inayomilikiwa na mfanyabiashara wa Lebanon, Samih Jamal, Vital Kamerhe amesema baadhi ya mikataba ilisainiwa bila ya yeye kupewa taarifa.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi juni 3 ambapo watashirikishwa mashahidi
Tayari Vital Kamerhe amekataliwa mara kadhaa kuachiliwa kwa dhamana, sawa na mfanyabiashara kutoka Lebanon ambaye amerejeshwa gerezani tangu mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya wiki kadhaa kufanyiwa matibabu katika mji mkuu wa Kinshasa.