Somalia yaadhimisha kumbukumbu ya miaka 60
Somalia imekuwa ikiadhimisha miaka 60 ya uhuru,ikiwa miongoni mwa mataifa ya Afrika Mashariki kuanza kujitawala, lakini raia wake wameendelea kuishi kwa shida huku wengi wakikimbilia katika nchi jirani ya Kenya.
Imechapishwa:
Eneo la Eastleigh jijini Nairobi ni mtaa ambao umekuwa nyumbani kwa maelfu ya raia wa Somalia. Wengi wanajihusisha na shughuli ya biashara, eneo hilo linafahamika kama Mogadishu ndogo.
Aden Ousman mkimbizi kutoka Somalia tangu mwaka 1991 amebaini kwamba Kenya ni nyumbani kushinda Somalia. Uhuru kwake hauna maana.
Hata hivyo amesema hatamani kurudi nyumbani hata iwapo hali itakuwa nzuri nchini Somalia.
Dhahir Duale mbunge wa Daadab, eneo wanakotoka wakimbizi wengi kutoka Somalia, amesema serikali ya Kenya na Somalia zina kibarua kuwatambua raia wa Somalia na Kenya.
Kwa upande wake Salah Abdi Sheikh mwandishi wa vitabu na mwanahistoria wa maswala ya Somalia anasema ana hofu kwamba nchi hiyo inapoteza zaidi kwa kuruhusu raia wake kuwepo kwenye mataifa mengine.
Somalia kwa zaidi ya miaka ishirini imekosa serikali imara baada ya kuzuka kwa ukosefu wa usalama kutokana na kundi la kigaidi la Al Shabab.