Uchaguzi wa urais: Guinea yaendelea kukumbwa na hali ya mvutano
Imechapishwa:
Tume ya uchaguzi huko nchini Guinea imeendelea kutangaza matokeo ya awali ya uchaguzi wa urais uliofanyika siku ya Jumapili. Haya yanajiri wakati chama kikuu cha upinzani cha UFDG, kimeahidi kufwata utaratibu wa kisheria kitakachotumia kudai ushindi wake.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Tume ya uchaguzi CENI huko Conakry hapo jana jioni, kura zilizohesabiwa kwenye majimbo manne kati ya38 katika nchi hiyo zimeonyesha kuwa rais anayemaliza muda wake Alpha Condé ndiye anayeongoza.
Haya ni matokeo ya mwanzo kwenye maeneo ya Matoto, Matam, Kaloum, katika mkoa wa Conakry na Boffa, katika mkoani Boké, msemaji wa tume hiyo amebainisha.
Haya yanajiri wakati hali ya wasiwasi imeendelea kushuhudiwa katika mji mkuu wa Guinea Conakry baada ya kikosi cha polisi kuvamia makazi ya kinara wa upinzani Cellou Dalein Diallo aliyejitangaza mshindi wa uchaguzi huo
Katika hatua nyingine, waangalizi wa kimataifa kutoka Umoja wa Afrika na ujumbe wa Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi ECOWAS wamesema kuwa uchaguzi wa urais uliofanyika nchini Guinea Conakry siku ya Jumapili iliyopita ulikuwa huru na wa haki.