Kipenga cha kampeni chapulizwa Burkina Faso, hali ya wasiwasi yatanda
Imechapishwa:
Kampeni za Uchaguzi Mkuu unaopangwa kufanyika Novemba 22 nchini Burkina Faso zinaanza leo Jumamosi Oktoba 31. Wagombea 13, ikiwa ni pamoja na rais anayemaliza muda wake na mwanamke mmoja watashiriki katika kinyang'anyiro hicho cha urais.
Kampeni hizi zinafanyika katika hali tete ya kiusalama. Nchi hiyo ina karibu watu milioni moja, wakimbizi wa ndani, waliolazimika kuyahama makaazi yao kufuatia mashambulio yanayotekelezwa na makundi ya yakijihadi.
Maeneo kadhaa ya baadhi ya mikoa yanakabiliwa na ukosefu wa usalama, moja ya changamoto kwa wagombea ni kwenda kukutana na watu hawa ambao wanahisi wametengwa.
Kwa kuanza kampeni hizi, wagombea kadhaa wameamua kwenda kukutana na watu wanaoishi katika maeneo ambayo yanashambuliwa na makundi yenye silaha. Kwa mfano, Kadré Désiré Ouédraogo, wa chama cha Agir Ensemble, amepanga kuanza kampeni yake katika mji wa Kaya kabla ya kuelekea mkoa wa Sahel.
Naye Zéphirin Diabré, kutoka chama cha Umoja wa Maendeleo na Mabadiliko (Union pour le progrès et le changement), baada ya mji wa Tenkodogo, katikati-Mashariki, ataelekea katika mkoa wa Mashariki. Na hapa ndipo timu ya rais wa zamani Yacouba Isaac Zida itaanzia kampeni yake.
"Hawana chaguo jingine, zaidi ya kwenda kwenye maeneo haya, ikiwa wana nia ya kuonyesha wapiga kura kwamba vita dhidi ya ukosefu wa usalama na ugaidi ni sehemu ya kipaumbele chao", amebaini mwanasayansi wa siasa Abdoul Karim Saïdou, mwalimu wa Chuo Kikuu cha Thomas Sankara.