Wafanyakazi zaidi ya 10 wa Umoja wa Mataifa kutoka Ethiopia wakamatwa Addis Ababa
Walikamatwa wakati wa operesheni zilizowalenga watu wa jimbo la Tigray kama sehemu ya hali ya hatari inayoendelea nchini Ethiopia, shirika la habari la AFP limeripoti Jumanne, likinukuu vyanzo vya Umoja wa Mataifa na kibinadamu.
Imechapishwa:
"Baadhi yao walikamatwa wakiwa majumbani mwao," kimeongeza moja ya vyanzo vya AFP. Msemaji mmoja mjini Geneva amesema Umoja wa Mataifa umeitaka wizara ya mambo ya nje ya Ethiopia kuwaachilia huru mara moja na bila masharti.
Umoja wa Mataifa unakadiria kuwa watu 400,000 katika jimbo la Tigray wanakabiliwa na kitisho cha baa la njaa.
Wakati huo huo Umoja wa Afrika na Marekani wamesema wanaona kuna nafasi ndogo ya fursa ya vita vya Ethiopia kumalizwa, wakati Umoja wa Mataifa ukitahadharisha juu ya nchi hiyo kutumbukia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe
Mjumbe wa Umoja wa Afrika katika pembe ya Afrika, Rais wa zamani wa Nigeria Olusegon Obasanjo pamoja na mjumbe wa masuala ya kisiasa wa Umoja wa Mataifa Rosemary DiCarlo wote walitoa taarifa kwa baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Obasanjo amesema hadi kufikia mwisho wa wiki hii, wanatarajia kuwa na mpango wa jinsi ya kusafirisha misaada ya kiutu na uondoaji wa wanajeshi ili kuridhisha pande mbili zinazohasimiana.