Marekani yaendelea kukumbwa na janga la Corona
Marekani ambayo imethibitisha visa 81,000 vya maambukizi ya virusi vinavyo sababisha ugonjwa hatari wa Covid-19, kwa sasa inazidi Italia na hata China kwa idadi ya visa vya maambukizi, kulingana na Gazeti la New York Times.
Imechapishwa:
Hali hiyo inayoendelea kushuhudiwa nchini Marekani inaonekana haimtishi Donald Trump, ambaye amesema anajianda kutaka "kufungua tena" nchi yake kwa sherehe za Pasaka, wakati wengi wameendelea kuomba hatua ya kuwataka raia waendelee kukaa nyumbani itumike katika nchi nzima ya Marekani.
Kulingana na Gazeti la New York Times, New York, ni kitovu cha janga la Corona nchini Marekani.
Katika jimbo hilo la New York, hatua ya kutotoka nje inaendelea kutumika, huku meya wa jimbo hilo akipiga marufuku kuendesha gari kwenye mitaa ya jiji. Lakini majimbo mengine bado hayajachukuwa hatua za kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo hatari.
Vyombo vya habari vinatabiri kuwa hali hiyo inatarajia kuwa mbaya kama ilivyo nchini China, au zaidi ya China.
"Ikiwa hawatachukuwa hatua hizo, Wuhan itahamia hapa New York, Wuhan huko Seattle, Wuhan huko Florida Kusini, na kadhalika, ametabiri mtaalam wa majanga kutoka gazeti wa New York Times, Donald McNeil Junior, katika makala ya gazeti lake la kila siku la Daily. Kwa sababu hospitali zitazidiwa kila mahali. Nimekuwa nikitazama hali hiyo tangu mwishoni mwa mwezi Januari na mwanzoni mwa mwezi Februari, na ilinitia hofu. Hii ni hali ya kutisha. Na sijaona mtu yeyote akichukulia maanani hali hii. Lakini huko ndiko tunakoelekea, " Donald McNeil Junior ameongeza.
Serikali ya Marekani imetuma barakoa 400 kwa jimbo la New York pekee, wakati kunahitajika barakoa 30,000. Kufikia sasa, wastaafu na wanafunzi 40,000 katika sekta ya afya wamejitolea kuimarisha timu za matabibu.