WHO yakutana na wanachama wake kujadili kuhusu Corona
Imechapishwa: Imehaririwa:
Nchi 194 wanachama wa Shirika la Afya Duniani, WHO, zinatarajiwa kupitisha kwa makubaliano azimio lililowasilishwa na Umoja wa Ulaya, ambalo linatoa wito wa kufanyika uchunguzi huru kwa hatua za shirika hilo tangu kuzuka kwa janga la Corona mwishoni mwa mwezi Desemba nchini China.
Marais, viongozi wengi wa serikali na mawaziri wanatarajia kila mmoja kutoa hoja yake katika Mkutano huu wa kimataifa wa afya, chombo cha maamuzi cha shirika la Umoja wa Mataifa, mkutano ambao unafunguliwa leo na utamalizika kesho Jumanne saa sita mchana.
Licha ya kuongezeka kwa mvutano kati ya Washington na Beijing, nchi hizo zina matumaini ya kupitisha kwa pamoja azimio refu lililowasilishwa na Umoja wa Ulaya. azimio hilo linaomba kuzindua "haraka iwezekanavyo (...) mchakato wa tathmini" kuchunguza udhibiti wa mgogoro wa kiafya kimataifa na hatua zilizochukuliwa na Shirika la Afya la Duniani, WHO, dhidi ya janga hilo.
Nakala hiyo pia inatowa wito kwa WHO "kushirikiana kwa karibu na Shirika la Afya ya Wanyama Duniani, Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula na Kilimo na nchi (...) kubaini chanzo cha virusi vya Corona na kubaini ni kwa njia gani viliingia kwa binadamu.