Clinton au Trump ? Raia wa Marekani waamua
Imechapishwa: Imehaririwa:
Raia wa Marekani wanapiga kura kumchagua rais mpya atakayewaongoza kwa muda wa miaka minne ijayo.
Mamilioni ya wananchi wa taifa hilo wanaamua kati ya Mfanyibiashara maarufu na tajiri Donald Trump au Bi.Hillary Clinton ambaye amewahi kuwa Waziri wa Mambo ya nje.
Bi.Clinton wa chama cha Democratic ikiwa atachaguliwa ataweka historia ya kuwa mwanamke wa kwanza kuwahi kuchaguliwa kuwa rais wa taifa hilo lenye nguvu duniani.
Trump naye anayewania wadhifa huo kwa chama cha Republican akifanikiwa kupata ushindi, atakuwa rais wa kwanza mfanyibiashara asiye na uzoefu wa kisiasa kuongoza taifa hilo.
Uchaguzi huu unaangaziwa kwa makini sana duniani hasa baada ya kampeni yenye nguvu kati ya wagombea hao kumalizika siku ya Jumatatu, huku wagombea hao wawili wakiwarai wapiga kura kuwachagua.
Wakaazi wa majimbo ya Mashariki yanayopakana na Bahari ya Atlantic ndio waliokuwa wa kwanza kuanza kupiga kura na katika vituo mbalimbali, foleni ndefu za wapiga kura zimeshuhudiwa.
Matokeo ya mwisho ya urais yanatarajiwa kufahamika kufikia mapema siku ya Jumatano.
Kuelekea kwenye uchaguzi huu, kura ya maoni zilikuwa zinaonesha kuwa Bi.Clinton alikuwa anaongoza lakini Trump aliendelea kusalia kuwa tishio.
Kabla ya siku ya kupiga kura, Wamarekani wengine zaidi ya Milioni 40 walikuwa wameshapiga kura katika zoezi la mapema lililomalizika Jumamosi iliyopita.
Mgombea anastahili kupata angalau kura 270 za wajumbe kati ya 538 ili kuwa rais wa Marekani na wajumbe hao huamua mshindi kwa namna watu walivyopiga kura katika majimbo mbalimbali.
Wakati wa uchaguzi wa mwaka 2012, Barrack Obama alipata ushindi baada ya kuchaguliwa kwa kupata kura 65,915,795 huku mpinzani wake Mitt Romney akipata kura 60,933,504.
Wajumbe walipopiga kura, Obama alipata ushindi wa wajumbe 332 dhidi ya Romney aliyepata kura ya wajumbe 206 katika uchaguzi huo.