George Floyd aagwa Minneapolis
Imechapishwa:
Familia, viongozi wa kidini, wanasiasa na watu mashuhuri wamekusanyika katika Chuo Kikuu cha North Central huko Minneapolis katika Ibada ya kuaga mwili wa George Floyd, mmarekani mweusi aliyefariki dunia akiwa mikononi mwa polisi.
Ibada hiyo ilifanyika Alhamisi zaidi ya wiki moja tangu kifo chake kilipozusha maandamano makubwa ya umma kote nchini Marekani.
Ibada hiyo ya kumbukumbu imeongozwa na mwanaharakati wa haki za kiraia Al Sharpton mjini Minneapolis, eneo ambalo Floyd alikufariki dunia baada ya kukandamizwa shingoni na polisi Mmarekani mweupe Mei 25.
Tayari waendesha mashtaka katika Jimbo la Minessota wamefungua kesi ya mauaji dhidi ya polisi huyo na wenzake watatu waliomkamata Floyd karibu na mkahawa mmoja wakidai alitaka kufanya manunuzi kwa kutumia fedha bandia.
Katikati mwa wiki hii Mwendesha mashtaka anayechunguza kifo cha George Floyd huko Minneapolis alisema Mmarekani huyo mweusi aliuawa kwa maksudi mwishoni mwa mwezi uliyopita.
Afisa wa polisi, mwenye umri wa miaka 46, aliyesababisha kifo chake kwa kumbana shingoni kwa goti lake ameshtakiwa kwa "mauaji yasiyokuwa ya kawaida" na maafisa wengine watatu waliokuwepo wakati wa George Floyd alipokamatwa, wameshtakiwa kwa kula njama kwa tukio hilo.
Awali Derek Chauvin, afisa wa zamani wa polisi alishtumiwa kwa mauaji bila kuksudia, na kwa sasa anakabiliwa na kifungo hadi miaka 40 dhidi ya kifungo cha miaka 25 kwa kosa la hapo awali.
Kwa kuongezea mashtaka yake, mwendesha mashtaka Keith Ellison, anayewakilisha mamlaka ya serikali ya Minnesota, ameongeza dhamana ya afisa huyo wa zamani hadi dola milioni moja.
Maandamano ya kupinga kifo cha Floyd na ukandamizaji wa polisi dhidi ya jamii ya watu weusi bado yanaendelea nchini Marekani lakini miji ya Los Angeles na Washington imeshuhudia kupungua kwa vurugu zilizosabishwa na waandamanaji.