Taiwan

Taiwan yaiwekea vikwazo Ufilipino

Rais wa Ufilipino Enigno Aquino
Rais wa Ufilipino Enigno Aquino gov.ph

Serikali ya Taiwan imewawekea vikwazo raia wa Ufilipino wanaoishi nchini humo kwa kusitisha mpango wa kuwaajiri baada ya mvuvi raia wa Taiwan kuuliwa nchini Ufilipino

Matangazo ya kibiashara

Taiwan imechukua hatua hiyo licha ya rais wa Ufilipino Enigno Aquino kuomba msamaha  kwa uongozi wa nchi hiyo.

Rais Aquino alimtuma mjumbe wa serikali Amadeo R. Perez kuomba msamaha huo na kuahidi kuwa serikali jijini Manila ilikuwa inashughulikia suala hilo kikamilifu.

Wiki iliyopita mvuvi huyo mwenye umri wa miaka 65 alipigwa risasi na kuuwawa baada ya kutuhumiwa na askari wa Ufilipino kuwa alikuwa anafanya uvuvi katika maji yao kinyume na sheria.

Waziri mkuu wa Taiwan Jiang Yi-huah amesema kuwa serikali yake ilipokea msamaha wa Ufilipino lakini mauaji yaliyotekelezwa dhidi ya raia wake hayakubaliki na hivyo ametoa wito kwa raia wa taifa lake kutozuru Ufilipino.

Aidha Taiwan imemwagiza balozi wake nchini Ufilipino kurudi nyumbani hatua ambayo inaonekana kudhoofisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Manila na Taipei.