Hali bado ni tete jijini Hong Kong licha ya kufikiwa kwa makubaliano
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hali imeendelea kuwa tete hii leo Ijumaa huko Hong Kong ambako wanaharakati wa mageuzi ya kidemokrasia wamepambana na polisi kwenye jiji hilo, licha ya makubaliano kufikiwa kati ya viongozi na wanafunzi wa vyuo vikuu juu ya kuanzisha mazungumzo.
Idadi kubwa ya waandamanaji waliokuwa wamekusanyika kwa wingi mbele ya ofisi za makao makuu ya bunge wamerejea makao mapema leo asubuhi, huku wengine kadhaa wakiwa bado katika eneo hilo.
Makao makuu ya serikali katika eneo hilo koloni zamani la Uingereza, limekuwa eneo la mkusanyiko wa waandamanaji waliomiminika barabarani tangu jumapili wakidai mabadiliko ya kidemokrasia.
Vuguvugu hilo linalo taka mageuzi ya kidemokrasia linaomba uwepo wa mazingira ya uchaguzi kwa kupiga kura wa moja kwa moja, na kujiuzulu kwa kiongozi wa jiji la Hong Kong Leung Chun Ying anaye chukuliwa na waandamanaji kama kibaraka wa utawala wa Pekin.
Waandamanaji wengi hawaamini kama mazungumzo yanaweza kufikia muafaka kutokana na msimamo wa kiongozi wa Hong Kong ambaye ametupilia mbali uwezekano wa kujiuzulu, huku serikali ya Pekin ikiweka bayana kwamba haitotimiza madai ya waandamanaji wanaotaka mageuzi.
Serikali ya Pekin inaona kwamba maandamano na madai hayo sio halali.