Ishirini na mbili wauawa katika mlipuko wa kemikali China
Imechapishwa:
Takriban watu ishirini na mbili wameuawa na wengine 22 kujeruhiwa katika mlipuko wa lori iliyokuwa inabeba bidhaa za kemikali mbele ya kiwanda kimoja nchini China.
Tukio hilo limetokea Jumatano wiki hii katika mji utakaopkea mashindano ya Michezo ya Olimpiki ya majira ya baridi mnamo mwaka 2022, kwa mujibu wa viongozi na vyombo vya habari nchini China.
Malori 38 na magari 12 yameharibika kutokana na mlipuko huo kufuatia kuzuka kwa moto mbele ya kiwanda cha Hebei Shenghua Chemical Group katika mji wa Zhangjiakou, kilomita 200 kaskazini magharibi mwa Beijing, manispaa ya mji huo imetangaza kwenye mtandao wa kijamii wa Weibo.
Watu waliojeruhiwa wamepelekwa katika hospitali baada ya mlipuko huo uliotokea saa 00:41 saa za China (sawa na saa 10:41 siku ya Jumanne saa za kimataifa), taarifa hiyo imesema.
Tukio hilo lilitokea kwenye lango la kiwanda, wakati gari lililobeba bidhaa hatari lililipuka, na kusababisha magari kadhaa kuharbika, shirika la Habari la China News limesema, likinukuu manispaa ya jiji la Zhangjiakou. Televisheni ya serikali CCTV imesema gari lililolipuka lilikua "lori la mafuta".