Annan afanya mazungumzo na Rais Assad huku Umoja wa Mataifa UN ukisema wengi waliouwa walichinjwa kule Houla
Imechapishwa:
Mpatanishi wa Kimataifa kutoka Umoja wa Mataifa UN na Jumuiya ya nchi za Kiarabu kwenye mgogoro wa Syria Kofi Annan amefanya mazunbumzo na Rais Bashar Al Assad yaliyojiegemeza kuangalia namna ya kutekeleza mpango wa amani ambao ameupendekeza ili kumaliza umwagaji damu.
Mkutano huo unakuja wakati Tume ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa UN ikisema wengi wa watu waliouawa kwenye mauaji ya kinyama ambayo yalifanyika katika eneo la Houla lililopo kwenye Jiji la Homs walichinjwa.
Msemaji wa Tume ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa UN Rupert Colville amesema watu ishirini pekee kati ya wale mia moja na nane ambao wameuawa ndiyo wamebainika kupigwa risasi lakini waliosalia ni waliochinjwa.
Colville amesema mashuhuda na manusura waliohojiwa wamesema wengi wa waliopoteza maisha katika eneo la Taldu walikuwa wamechinjwa na watu ambao hadi sasa hawajajulikana licha ya uchunguzi kuendelea.
Msemaji huyo wa Tume ya Haki za Binadamu ameongeza kila kitu kipo wazi kwenye uchunguzi ambao wameufanya na umebainisha watu hao hawakuuawa kwa kupigwa risasi tu kama ambavyo ilielezwa awali.
Taarifa hii ya Tume ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa UN inakuja wakati huu ambapo Uingereza, Ujerumani, Ufaransa na Australia kila mmoja kwa muda wake wamewatimua Wanadiplomasia wa Syria kuonesha kupinga utawala uliopo madarakani.
Chanzo cha Habari kutoka Serikali ya Uingereza zimeeleza hatua ya kuwatimua Wanadiplomasia hao na taarifa zaidi zinatarajiwa kutolewa baadaye na Waziri wa Mambo ya Nje William Hague.
Baraza la Mpito la Upinzani nchini Syria limepokea kwa shauku hatua ya kutimuliwa kwa Wanadiplomasia kutoka nchi za Ufaransa, Uingereza, Ujerumani na Australia huku kukiwa na tetesi Marekani nayo huenda ikafuata nyyo za nchi hizo.