TANZANIA-BIASHARA

Uchunguzi waanzishwa kwa wafanyabiashara wa Sukari Tanzania

Serikali ya Tanzania kupitia Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU imeanzisha uchunguzi dhidi ya wafanyibiashara wanaokabiliwa na tuhuma za kuficha sukari nchini na kusababisha usumbufu kwa jamii kwa kupanda kwa gharama ya bidhaa hiyo.

John Pombe Magufuli, Rais mpya wa Tanzania, Oktoba 30, 2015.
John Pombe Magufuli, Rais mpya wa Tanzania, Oktoba 30, 2015. REUTERS/Sadi Said
Matangazo ya kibiashara

TAKUKURU imekagua mabohari ya wafanyabiashara wakubwa wa sukari jijini dar es salaam ikiwemo ya bwana Harun Daudi Zakaria iliyoko tabata na kubaini jumla ya tani elfu nne na mia tano iliyonunuliwa kutoka kiwanda cha sukari cha kilombero.

Kwa kushirikiana na jeshi la polisi TAKUKURU imebaini kuwepo kwa mikakati ya wafanyabiashara wa ndani kununua sukari na kuihifadhi na kuuza bidhaa hiyo kidogo kidogo kwa siku tani 250.

Kuficha bidhaa ni kosa la kuhujumu uchumi nchini Tanzania kwa mujibu wa sheria ya uhujumu uchumi sura ya 200 chapisho la mwaka 2002.