Baraza la seneti la Kenya kujadili mabadiliko ya sheria ya Uchaguzi
Imechapishwa:
Maseneta nchini Kenya wanakutana leo kujadili na kuyapigia kura mabadiliko ya sheria ya Uchaguzi kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka 2017.
Hatua hii imekuja baada ya bunge la Kitaifa kufanikiwa kuibadilisha sheria hiyo wiki iliyopita.
Mabadiliko hayo yanairuhusu Tume ya Uchaguzi kutumia mfumo wa kawaida, kuwatambua wapiga kura na kujumuisha matokeo, ikiwa mfumo wa eletroniki utagoma kufanya kazi mabadiliko yanayopingwa na upinzani.
Kiongozi wa upinzani Raila Odinga ameipa serikali siku nane, kuja katika meza ya mazungumzo kujadili suala hili la sivyo, kutakuwa na maandamano ya nchi nzima tarehe 4 mwezi Januari mwaka 2017.
Maaskofu wa Kanisa Katoliki, na viongozi wengine wa dini pia wamejitokeza na kumtaka rais Uhuru Kenyatta kutokubali mabadiliko hayo na kutoa nafasi ya kuwepo kwa mazungumzo ya kisiasa.