KENYA

Mahakama ya juu nchini Kenya yatupilia mbali ushahidi mpya uliowasilishwa na muungano wa CORD

Mahakama ya juu nchini Kenya imetupilia mbali ombi lililowasilishwa na muungano wa CORD kuhusu kutaka kufanyika kwa uchunguzi wa kisayansi kwenye mitambo yote ya IEBC iliyotumika katika kusajili wapiga kura. 

Jopo la majaji wa mahakama ya juu nchini Kenya wanaotarajiwa kutoa uamuzi kuhusu kesi za kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwezi March mwaka huu
Jopo la majaji wa mahakama ya juu nchini Kenya wanaotarajiwa kutoa uamuzi kuhusu kesi za kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwezi March mwaka huu Reuters
Matangazo ya kibiashara

Majaji wanaosikiliza kesi hiyo wamesema kuwa kulingana na muongozo wa katiba ya Kenya muda uliotolewa kisheria kwa mahakama hiyo kutoa hukumu hautatosha kuruhusu pia uchunguzi wa kisayansi kufanyika kwenye mitambo ya IEBC.

Katika hatua nyingine, majaji hao pia wamekataa kuijumuisha taasisi ya katiba kama rafiki wa mahakama kwenye kesi hiyo kwa kile ilichoeleza kuridhishwa na upande wa utetezi kuwa kujumuishwa kwao huenda kukaathiri mwenendo wa kesi.

Hata hivyo majaji wanaoongozwa na daktari Willy Mutunga ualiamua kuwa siku ya Jumanne ndio watatangaza uamuz wao kabla ya kuanza rasmi kusikilizwa kwa pingamizi zilizowasilishwa siku ya Jumatano.

Majaji wa mahakama ya juu nchini Kenya wanaosikiliza kesi zilizowasilishwa kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika nchini humo tarehe 4 March mwaka huu, wameagiza kurudiwa kuhesabiwa upya kwa kura kwenye vituo 22.

Uamuzi wa majaji hao ukiongozwa na rais wake Daktari Willy Mutunga umeagiza kurejelewa upya kwa zoezi la uhesabuji wa kura kwenye vituo 22 vya kupigia kura kuhakiki iwapo idadi ya waliopiga kura walizidi idadi ya watu waliojiandikisha.

Muungano wa CORD unaoongozwa na waziri mkuu Raila Odinga uliwasilisha utetezi wake mbele ya jopo hilo la majaji wakionesha kuwa katika baadhi ya maeneo idadi ya wapiga kura ilizidi ile idadi ya wananchi waliojiandikisha na hivyo kumuongezea kura rais mteule Uhuru Kenyatta.

Akitangaza uamuzi huo, jaji Mtunga amesema kuwa kuamuru kuhesabiwa upya kwa kura hizo ni kutaka mahakama kujiridhisha iwapo ni kweli idadi ya waliojiandikisha ilizidi ile ya waliopiga kura.

Mahakama imeiagiza tume ya uchaguzi na ukaguzi wa mipaka IEBC kuhakikisha inarudia zoezi hilo na kuwasilisha matokeo yake siku ya Jumatano.

Katika hatua nyingine majaji hao pia wameagiza kufanyika uchunguzi wa kina na wakisayansi katika stakabadhi namba 34 ambayo muungano wa CORD unadai kuwa kulikuwa na ukiukwaji mkubwa wa ujazwaji wa stakabadhi hiyo jambo ambalo limechangia kushindwa kwenye uchaguzi uliopita.

Awali mawakili wa pande zote mbili walikuwa wakivutana kuhusu ushahidi mpya uliowasilishwa na kodi wenye zaidi ya kurasa elfu mmoja huku mawakili wanaomwakilisha Uhuru Kenyatta wakitaka majaji kutupilia mbali madai ya upande wa mashtaka.

Majaji hao pia wamekubali kumjumuisha mwanasheria mkuu wa Serikali Githu Mungai kama rafiki wa mahakama na kutupilia mbali ombi la chama cha wanasheria nchini humo kujumuika kama rafiki wa mahakama kwenye kesi hiyo.