Trump kukutana na Mahmoud Abbas Jumanne hii
Imechapishwa:
Rais wa Marekani Donald Trump anatarajiwa kukutana na kiongozi wa Mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas, Jumanne hii ni siku ya pili ya ziara yake katika eneo la Mashariki ya Kati, baada ya kukutana siku ya Jumatatu na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu pamoja na rais wa nchi hiyo.
Ziara hiyo ya siku mbili nchini Israel na katika utawala wa Palestina ni sehemu ya ziara ya kwanza ya kigeni ya bwana Trump.
Rais Trump anajitambua kama mpatanishi mkuu wa kutatua masuala ambayo yamewashinda watu wengi.
Suala kuu ni kubuniwa kwa taifa huru la palestina kando ya Israel.
Eneo la ukingo wa Magharibi pamoja na mashariki mwa mji wa Jerusalem limekaliwa na Israeli kwa miaka 50.
Baadhi ya watu wenye ushawishi ndani ya serikali ya Israel wanaamini kuwa ardhi hiyo ni ya Waisraeli waliyopewa na Mwenye Enzi Mungu.
Siku ya Jumatatu Trump alisema kuwa kuna ushirikiano mkubwa kati ya Marekani na Israel, huku akionya juu ya kuwepo kwa tishio la Iran kwa usalama wa dunia
Itafahamika kwamba Israel na Palestina hawajafanya mazungumzo ya moja kwa moja kwa zaidi ya miaka mitatu.