Urusi, Iran na Uturuki wakubaliana kuleta pamoja serikali ya Syria na upinzani mjini Sochi
Imechapishwa:
Mkutano wa kilele wa Sochi kuhusu mchakano wa amani nchini Syria ulimalizika jana Jumatano jioni nchini Urusi. Vladimir Putin aliwapokea katika mji wa Sochi marais wenzake wa Iran na Uturuki.
Viongozi hao watatu ambao ni wadhamini wa mchakano wa Astana walisema mkutano huo una lengo la kuiandaa Syria baada ya "vita vya wenyewe kwa wenyewe".
Vladimir Putin alitangaza kwamba walikubaliana na wenzake kutoka Iran na Uturuki kufanyika kwa mkutano ujao nchini Urusi, mkutano ambao utawaleta pamoja serikali ya Syria na upinzani.
Mkutano huo wa Sochi ulimalizika kwa tangazo la pamoja kwamba Urusi, Uturuki na Iran wanataka kuleta pamoja upinzani wa Syria na serikali ili kuiondoa nchi hiyo katika mgogoro wa kisiasa unaoendelea.
Vladimir Putin alifanya kazi kubwa ya kujaribu kuzileta pamoja pande hasimu katika mgogoro wa Syria kwa kuwashawishi wenzake Reccep Tayyip Erdogan na Hassan Rohani.