Kivumbi cha kumtafuta bingwa wa soka kwa wanawake barani Afrika kuanza
Michuano ya soka kutafuta bingwa wa makala ya 12 ya mashindano ya timu za taifa kwa upande wa wanawake barani Afrika, inafunguliwa Jumamosi katika uwanja wa Ahmadou Ahidjo jijini Yaounde nchini Cameroon.
Imechapishwa:
Wenyeji (Indomitable Lionesses) ambao wanashiriki katika michuano hii kwa mara 11, watafungua dimba dhidi ya Misri saa kumi na moja na nusu jioni saa za Afrika Mashariki.
Misri inashiriki katika michuano hii kwa mara ya pili, mara ya mwisho ikiwa ni mwaka 1998, na kuondolewa katika hatua ya makundi.
Mataifa nane yanashiriki katika michuano hii na yamewekwa katika makundi mawili.
Kundi la A: Cameroon, Misri, Afrika Kusini na Zimbabwe
Kundi la B: Nigeria, Mali, Ghana na Kenya.
Siku ya Jumapili mabingwa watetezi Nigeria na ambao wameshinda taji hili mara saba watafungua michuano hii dhidi ya Mali mjini Limbe kuanza kusaka taji la nane.
Kocha wa Super Falcons, Florence Omagbemi amesema matarajio ni makubwa lakini chochote kinaweza kutokea kwa sababu kila timu inataka kuifunga Nigeria.
Hii ndio mara ya kwanza kwa Florence kuwa kocha baada ya kustaafu kucheza soka na kuwa nahodha, alipoisadia nchi yake kushinda mataji 4.
Kenya ambayo inashiriki katika michuano hii kwa mara ya kwanza, itamenyana na Ghana ambayo imeshiriki katika michuano hii mara 11 na kumaliza katika nafasi ya pili mara tatu mwaka 1998, 2002 na 2006.
Ratiba ijayo kundi A Jumanne Novemba 22 2016
- Cameroon vs Afrika Kusini
- Zimbabwe vs Misri
Ratiba ijayo ya kundi B Jumatano Novemba 23 2016
- Nigeria vs Ghana
- Kenya vs Mali