Serena na Venus Williams kumenyana katika fainali ya Australian Open
Imechapishwa:
Serena Williams atamenyana na dada yake Venus Williams katika fainali ya kuwania taji la mwaka huu la mchezo wa Tennis la Australian Open, kwa upande wa wanawake.
Makala ya 105 ya michuano hii inaendelea jijini Melbourne na fainali hiyo itachezwa siku ya Jumamosi.
Hii itakuwa fainali ya 9 kwa wawili hao kukutana katika historia ya michuano mikubwa ya Tennis duniani, tangu walipoanza kucheza mchezo huu.
Venus mwenye umri wa miaka 36, alifuzu katika hatua ya fainali baada ya kumshinda Mmarekani mwenzake Coco Vandeweghe katika mchezo wa nusu fainali kwa seti za 6-7 (3-7) 6-2 6-3.
Hii ndio fainali ya kwanza ya Venus anayeorodheswa wa 13 duniani kwa upande wa wanawake kufika katika hatua hii tangu mwaka 2009.
Serena mwenye umri wa miaka 35, ambaye anaorodheswa kama mchezaji wa pili kwa ubora duniani, alimshinda mpinzani wake kutoka Croatia, Mirjana Lucic-Baroni kwa seti za 6-2 6-1 na kufuzu katika hatua hiyo.
Ikiwa Serena Williams atashinda taji la mwaka huu, litakuwa taji lake la saba la Australian Open, huku Venus akishinda taji hilo, litakuwa taji lake la nane.