Mzozo wa kisiasa watokota Brazil
Imechapishwa:
Nchi ya Brazil inashuhudia mzozo wa kisiasa baada ya wabunge kupitisha mswada wa kukosa imani na rais Dilma Rousseff.
Hatua hii imepokelewa kwa furaha kubwa na wapinzani nchini humo wanaomtuhumu Rais Rousseff kutumia fedha za umma wakati wa kampeni za kisiasa mwaka 2014.
Serikali imelaani hatua hiyo ya wabunge na kusema imechukuliwa bila ya ushahidi wowote kuwa Rais Dilma Rousseff alitumia vibaya fedha za serikali.
Bi. Rousseff mwenyewe amekuwa akisema kuwa wapinzani wake wanataka kumpindua kisiasa na anatarajiwa kuzungumzia hatua hiyo baadaye leo.
Kitakachofuatia, bunge la Senate mwezi ujao litapiga kura kuamua ikiwa rais Rousseff ashtakiwe na ikiwa itakuwa hivyo, ataondoka madarakani na nafasi yake kuchukuliwa na Makamu wake Michel Temer.