Rais wa Gambia aapa kutoachia ngazi katika uongozi wa nchi
Rais wa Gambia Yahya Jammeh amesisitiza kuwa hataondoka madarakani muhula wake utakapomalizika tarehe 19 mwezi Januari mwaka ujao.
Imechapishwa:
Jammeh ambaye amekuwa akisema kuwa mpinzani wake Adama Barrow aliyetangazwa mshindi hakushinda kwa haki, amesisistiza kuwa hatatishwa na yeyote.
Juhudi za viongozi wa nchi za Afrika Magharibi kumshawishi rais Jammeh kuondoka madarakani hazijafua dafu huku chama cha Jammeh kikiendelea Mahakamani kutaka Uchaguzi huo kufutwa.
Juma lililopita upinzani nchini Gambia ulionya kuwa endapo rais anayemaliza muda wake nchini humo Yahya Jammeh atakataa kuondoka Madarakani atachukuliwa kama muasi. Yahya Jammeh alirejelea kauli yake hivi karibuni baada ya kutambua ushindi wa mshindani wake Adama barrow, na kutaka kura zirudi kuhesabiwa upya.
Hivi karibuni Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa katika Afrika Magharibi, Mohamed Ibn Chambas, alisema kuwa Rais wa Gambia Yahya Jammeh anapaswa "kuwa tayari kukabidhi madaraka" ifikapo mwezi Januari mwakani.
Bw ibn Chambas alisema Umoja wa Mataifa hautaendelea kufumbia macho viongozi ambao hushindwa na kisha baadaye wanatumia nguvu kwa kuchukua madaraka.
"Upinzani ulishinda uchaguzi, ambao uliku halali, " amesema Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa wa Ban Ki-moon katika Afrika ya Magharibi.
Jumanne Desemba 13 Marais wanne kutoka Afrika Magharibi walifanya ziara katika mji mkuu wa Gambia, Banjul na kujaribu kumshawishi Yahya Jammeh kukubali kushindwa katika uchaguzi wa urais na kukabidhi madaraka, bila mafanikio.
Mihula ya miaka mitano ya Bw Jammeh itamalizika Januari 19, Mohamed Ibn Chambas amesema, huku akiongeza kuwa "atakuwa tayari kukabidhi madaraka" tarehe hiyo.