Ukraine: waasi wadai kuuteka mji wa Debaltseve
Mapigano yanaendelea kurindima nchini Ukraine wakati ambapo baadhi ya viongozi wa Ulaya na Marekani walikutana Jumanne wiki hii mjini Minsk na kuafikiana kuhusu kusitishwa kwa mapigano mashariki mwa nchi hiyo, na namna ya kudhibiti hali ya machafuko inayoendelea.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wakati huohuo waasi wanaotaka kujitenga kwa eneo la mashariki wametangaza kuuteka mji wa Debaltseve, lakini raia wa Ukraine wamebaini kwamba mapigano bado yanaendelea pembezoni mwa mji huo muhimu.
Vikosi vya Ukraine katika mji wa Debaltseve wanasadikiwa kuwa wamezingirwa na waasi, ambao wamesema kuwa wameteka barabara kuu muhimu zinazoingia katika mji huo. Mji wa Debaltseve unapatikana kati ya majimbo ya Donetsk na Lougansk, ambayo yako chini ya udhibiti wa waasi wanaotaka kujitenga kwa eneo la mashariki mwa Ukraine. Mji huo ni muhimu pia kwa waasi , kwani unaunganisha eneo la mashariki la Ukraine na Urusi. Hata hivyo viongozi wa kijeshi wa Ukraine wanathibitisha kwamba mapigano bado yanaendelea.
Mapigano ya Debaltseve ni ishara. Wakati majadiliano ndio yakianza katika mji wa Minsk kati ya wanadiplomasia kutoka Ukraine, Urusi, Ufaransa na Ujerumani, kila upande kati ya pande zote mbili katika mgogoro umekua ukitafuta nafasi katika mazungumzo hayo ili kuonesha nguvu ulizo nazo.
Viongozi wa waasi wanaotaka kujitenga kwa eneo la mashariki mwa Ukraine, wamekua wakibaini kwamba kamwe hawatokubali kusitisha mapigano, kabla ya kuudhibiti mji wa Debaltseve.
Makao makuu ya jeshi katika mji wa Kramatorsk, nchini Ukraine, yameshambuliwa kwa roketi Jumanne wiki hii, na kusababisha vifo vya watu sita.