Ndege ya Germanwings iliangushwa kwa makusudi
Imechapishwa:
Imethibitishwa kuwa mmoja wa marubani wa ndege ya Germanwings iliyoanguka kwenye milima ya Alps nchini Ufaransa na kuua watu wote 150 waliokuwemo kwenye ndege hiyo, alifanya makusudi kusabisha ajali hiyo baada ya kumfungua rubani mwenzake mlango.
Maofisa wa uchunguzi wa ufaransa, wamethibitisha kuwa rubani, Andreas Lubitz, alifunga mlango wa kuingia kwenye kichwa cha ndege hiyo na kubonyeza kitufe cha kuifanya ndege ianze kushuka kwa kasi ambapo kwa mujibu wa kisanduku cha sauti inaonesha alikusudia kutekeleza tukio hili.
Mwendesha mashtaka kiongozi wa Ufaransa, Brice Robin amesema kuwa wanafanya uchunguzi zaidi kubaini sababu za rubani huyo kufanya alichokifanya wakati huu polisi wakifanya uchunguzi kwenye nyumba yake ya mjini Frankfurt, Ujerumani.
Katika hatua nyingine, mashirika kadhaa ya ndege yametangaza kuchukua hatua za ziada kuzuia tukio kama hili kutokea ikiwa ni pamoja na kuweka milango ya marubani inayoweza kufunguka kwa nje, mpango ambao umeungwa mkono na mkurugenzi mtendaji wa shirika la ndege la Ujerumani, Lufthansa, Carsten Spohr licha ya kuwa baada ya kubanwa na waandishi wa habari alikuwa mkaidi na kukanusha sababu za ajali kuwa huenda zilitokana na mafunzo duni ya marubani wake.