Coronavirus: Zaidi ya kesi 186,000 za maambukizi zathibitishwa Ujerumani
Imechapishwa:
Idadi ya kesi za maambukizi ya virusi vya Corona zilizothibitishwa nchini Ujerumani imeongezeka hadi 186,022, baada ya kesi mpya 348 kuthibitishwa ndani ya kipindi cha saa 24, kulingana na takwimu zilizotolewa na Taasisi ya Robert Koch (RKI).
Vifo vipya 18 vimeripotiwa, kulingana na takwimu za RKI, kwa jumla ya vifo 8,781 tangu kuzuka kwa janga hilo nchini Ujerumani.
Hayo yanajiri wakati Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya imepatiwa mamlaka ya kisiasa kutoka kwa serikali za nchi wanachama ya kufanya mazungumzo kwa niaba yao kuhusu ununuzi wa mapema wa chanjo zinazoonyesha matumaini ya kupambana na virusi vya Corona.
Ujerumani, Ufaransa, Italia na Uholanzi wako tayari kwa mazunguzmo na makampuni ya dawa kununua chanjo hiyo, hatua ambayo huenda ikadhoofisha mpango huo wa pamoja wa Umoja wa Ulaya.